TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Mkoa wa Arusha 
imefanikiwa kuokoa zaidi ya Sh milioni 74.8 zilizolipwa kwa watumishi na
 semina hewa. Aidha watumishi wa umma wamesisitizwa kufanya kazi kwa 
maslahi ya umma, kwa kuzingatia suala zima la uadilifu na kuacha 
kuwashawishi wananchi kutoa fedha ili wapate huduma.
 
Hayo yalisemwa jana na Kaimu Kamanda wa Taasisi ya Kuzuia na 
Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Arusha, Frida Wikessy wakati 
alipotoa taarifa ya utendaji kazi wa tasisi hiyo katika kipindi cha 
Julai mwaka jana hadi Machi mwaka huu.
Wikessy alisema fedha hizo zimerejeshwa serikalini baada ya kuziokoa 
kutokana na watumishi hewa pamoja na semina hewa zilizoandikwa kwa 
kughushi saini ili watu wajipatie fedha. Alisema fedha hizo zilitokana 
na watumishi hewa Idara ya afya na elimu ambapo kulikuwa na watumishi 
wameacha kazi, kufa na wengine kuhama vituo vya kazi, lakini serikali 
iliendelea kulipa.
Aidha katika kipindi hicho mkoa huo ulipokea jumla ya malalamiko 248 
kwa njia mbalimbali na kati ya hayo majalada 24 ya uchunguzi 
yanaendelea, yapo katika hatua mbalimbali. Frida alisema katika uongozi 
wa awamu ya tano umekuwa na ongezeko la wananchi kutoa taarifa nyingi 
tofauti na miaka ya nyuma, hali inayosababisha kupokea malalamiko yalio 
sahihi na yasio sahihi. Pia alisema katika kipindi hicho mashauri 14 
yalisikilizwa na kati ya hayo 10 yalishinda katika kesi za jinsi na 
uhujumu uchumi

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni